Sunday, 26 February 2017

WANAHABARI WATIMULIWA IKULU MAREKANI (WHITE HOUSE)



IKULU ya Rais wa Marekani imeyazuia mashirika kadhaa makuu ya habari nchini humo kuhudhuria kikao cha wanahabari kilichoendeshwa na msemaji wa Ikulu, Sean Spicer.
Wanahabari wa Mashirika ya CNN, The New York Times, Politico, Los Angeles Times na BuzzFeed hawakuruhusiwa kuhudhuria kikao cha wanahabari katika ofisi ya Msemaji wa Ikulu ya Rais wa Marekani.
Wamelaani kitendo hicho na kukiita kuwa ni cha kibaguzi dhidi ya vyombo vya habari na wanahabari wenyewe. Utawala wa Rais Donald Trump umekuwa ukiyashutumu mashirika hayo kuwa yanaeneza habari za uongo na za kupotosha.
Spicer hakutoa maelezo; kwanini waandishi wa habari wa mashirika hayo waliachwa nje ya kikao kisicho rasmi cha wanahabari, hatua ambayo imeibua shutuma kali.
Shirika la Habari la Reuters pamoja na mashirika mengine 10 yakiwemo Bloomberg na CBS yaliruhusiwa kuhudhuria mkutano huo wa wanahabari.
Wakati wanahabari kutoka CNN na mashirika mengine yaliyoathiriwa yalipojaribu kuingia IKulu, yalizuiwa kwa kuambiwa majina yao hayako katika orodha ya wanahabari walioalikwa.
Katika mkutano wa wanaharakati wa kisiasa wa Jumuiya ya CPAC juzi, Rais Trump alivishutumu baadhi ya vyombo vya habari ambavyo anadai vinatoa taarifa za uongo na kuvitaja kuwa adui ya watu wa Marekani.
Spicer alisema kundi lake liliamua kufanya mkutano mdogo wa wanahabari katika ofisi yake badala ya mkutano rasmi wa wanahabari kama ilivyo desturi katika chumba cha wanahabari katika Ikulu ya Rais akihoji hawahitaji kuendesha kila kitu mbele ya kamera kila siku.
Wanahabari kutoka mashirika ya Associated Press na Jarida la Time waliondoka kutoka kwenye kikao hicho walipoarifiwa kuwa wanahabari wenzao kutoka mashirika mengine wamezuiwa kuhudhuria kikao hicho.
Taarifa kutoka kwa Mhariri Mkuu wa The New York Times; Dean Baquet ilisema jambo kama hilo halijawahi kutokea katika Ikulu ya Rais ya White House katika historia yao ndefu ya kuripoti taarifa kutoka tawala chungu nzima kutoka vyama tofauti vya kisiasa nchini Marekani.
Baquet alisema wanapinga kuzuiwa kwa gazeti lao na mashirika mengine ya habari na kuongeza kuruhusiwa kwa vyombo hivyo kuwa na uhuru na kuangazia matukio ya serikali iliyo wazi bila shaka ni muhimu kwa maslahi ya taifa.
Chama cha maripota wa Ikulu ya White House (WHCA) pia kimepinga hatua hiyo ya Spicer.
Rais wa chama hicho, Jeff Mason ambaye ni ripota wa Reuters alisema wanapinga jinsi kikao hicho kilivyoendeshwa na Ikulu ya White House.
Katika kipindi cha kampeni mwaka jana, kundi la Trump liliyapiga marufuku mashirika kadhaa likiwemo gazeti la Washington Post na Buzzfeed dhidi ya kuripoti katika mikutano ya kampeni likiyashutumu kwa upotoshaji na kueneza habari za uongo

No comments:
Write comments