Thursday 16 March 2017

Kebwe apiga marufuku usafirishaji mkaa Moro

MKUU wa Mkoa wa Morogoro, Dk Stephen Kebwe ameziagiza mamlaka za maliasili za misitu kushirikiana na vyombo vya dola kukamata magari yanayosafirisha mkaa kutoka mkoani huo na kubaini uhalali wake ili kudhibiti kuteketea kwa misitu.

Zaidi ya hekta 150,000 za misitu katika maeneo mbalimbali ya mkoa huo inaangamizwa kwa mwaka kutokana na uchomaji wa mkaa, kuni na mbao.

Alitoa agizo hilo wakati akizindua mashine za kisasa za kutengeneza kuni mkaa zilizoboreshwa chini ya Kampuni ya Demaco ya mkoani Morogoro. Mkoa wa Morogoro una misitu mingi ya hifadhi, vijiji na ile ya asili.

Kumekuwepo uharibifu na ukataji wa miti unaoathiri wilaya za mkoa huo jambo linaloweza kusababisha maeneo mengi ya mkoa huo kugeuka jangwa.

“Kuanzia sasa mkaa usitoke katika Mkoa wa Morogoro…,” alisema Dk Kebwe.

Mkurugenzi wa Demaco, Kaya Kazema alisema mashine za kutengeneza kuni mkaa kwa kutumia malighafi ya pumba za mpunga, unga wa makaa ya mawe na Allanbakia zitachangia kwa kiwango kikubwa kupunguza matumizi ya kuni asilia zinazotokana na ukataji wa miti

No comments:
Write comments