Thursday 1 June 2017

Balozi wa Marekani anena mazito kuhusu utawala wa sheria na haki Tanzania




Ofisa wa juu wa Ubalozi wa Marekani ana wasiwasi kutokana na jinsi viashiria vinavyokatisha tamaa, kuonyesha kwamba Tanzania inarudi nyuma katika masuala ya uwazi, haki za binadamu na utawala wa sheria na kusema visiposhughulikiwa, vitaathiri biashara na nafasi ya nchi kama kinara wa usalama.

Ofisa huyo, Virginia Blaser, Balozi Mdogo wa Marekani Afrika Mashariki, alisema hayo katika mahojiano maalumu na gazeti la The Citizen Alhamisi iliyopita, siku chache kabla ya kumaliza kipindi chake cha miaka minne.

Alisema wakati Serikali ikistahili pongezi kwa jitihada ilizoonyesha za kupambana na rushwa, pia inatakiwa ichukue hatua kuendeleza uwazi na utawala wa sheria na kuangalia ishara zinazotia shaka ya kurudisha nyuma mambo, hasa sekta binafsi.

“Mustakabali wa Watanzania hauwezi kutegemea wadau wa maendeleo; hautatokana na ajira za serikalini; unatakiwa utoke katika sekta binafsi ambayo ni pana, imara, yenye hali nzuri na inayoaminika,” alisema.

“Na badala yake, naona ishara zinazokatisha tamaa katika sekta binafsi; na nina wasiwasi Tanzania itachukua njia gani.”

Aliongeza kuwa angependa kuona kampuni nyingi zaidi kutoka Marekani zikiingia nchini, lakini hilo litategemea zaidi “mazingira ya uwazi na yanayosaidia sekta binafsi”

No comments:
Write comments