Wednesday 8 March 2017

JPM kupokea kifimbo cha Malkia


Rais John Pombe Magufuli atapokea kifimbo cha Malkia kwa ajili ya uzinduzi wa michezo ya Jumuiya ya Madola.

Kifimbo hicho kitazinduliwa Machi 13 nchini England na kuanza kukimbizwa katika maeneo mbalimbali duniani kabla ya kuwasili nchini Aprili 8.

Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Filbert Bayi alisema kifimbo hicho kitakimbizwa hapa nchini kwa siku mbili.

"Kifimbo cha Malkia kitakimbizwa Dar es Salaam na Arusha, ikiwa jijini Dar es Salaam kitakwenda Ikulu na kupokelewa na Rais Magufuli," alisema Bayi na kuongeza.

"Tayari TOC tumeanza maandalizi ya kukipokea kifimbo hicho kwa kushirikiana na Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Wizara ya mambo ya ndani na wizara ya mambo ya nje.

"Wanamichezo mbalimbali watakikimbiza kutoka Taifa kuelekea Ikulu siku ya Aprili 9 na siku inayofuata kitakwenda Arusha ambapo kitakimbizwa kabla ya kuondoka kuelekea nchi nyingine," alisema.

Kifimbo cha Malkia kinakimbizwa katika nchi zilizowahi kutawaliwa na Uingereza kwa ajili ya uzinduzi wa michezo ya madola ambayo itafanyika Aprili mwakani nchini Australia

No comments:
Write comments