Monday 12 June 2017

SUMAYE AFUNGUKA YA MOYONI ATAJA SABABU INAYOPELEKEA NCHI KUTOKUENDELEA

WAZIRI Mkuu Mstaafu na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Fredrick Sumaye, amesema nchi inashindwa kuendelea kwa sababu inaendeshwa kishabiki  na kwamba mambo yanayofanyika hayana maslai kwa taifa.
FREDRICK SUMAYE.
Akizungumza kwenye  Kongamano la Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha) na Umoja wa Vijana wa Vyuo Vikuu ambao ni wanachama wa Chadema (Chaso) jijini Mbeya alipokuwa mgeni rasmi, Sumaye alisema mambo mengi yenye masirahi ya taifa yakifanywa kimzaha yatasababisha madhara kwa taifa.
Sumaye ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani, alisema miongoni mwa mambo ambayo ni ya maslahi ya taifa lakini  yanendeshwa kishabiki ni mikataba ya madini na bajeti isiyokuwa na uhalisia.
Mengine aliyoyataja ni uendeshaji wa Bunge ambalo kikatiba ni chombo huru ambacho hakipaswi kuiingiliwa na wabunge kufanya maamuzi kwa maslahi ya vyama vyao vya siasa huku wengine wakishangilia na kuzomeana.
“Nchi kwa sasa inayumba na inashindwa kuendelea kutokana na kuendeshwa kishabiki, Bajeti yetu ya mwaka uliopita fedha za miradi ya maendeleo zilitolewa kwa asilimia 34 pekee na serikali ilikiri, lakini sasa hivi wanakuja na bajeti kubwa zaidi ya hiyo ambayo haijatekelezwa na wabunge wa CCM wanashangilia,” alisema Semaye na kuongeza:
“Mambo haya yanaliingiza taifa kwenye matatizo makubwa, deni la Taifa linazidi kuongezeka, mikataba ya madini na mingine iliyokuwa ni yenye maslahi ya taifa sasa inakuwa ni ya hasara kwetu, lakini ukiangalia wabunge wanapiga meza wakishangilia.”
Sumaye alisema wasomi wa vyuo vikuu hawatumiki ipasavyo kwa maslahi ya taifa ikiwamo kujadili mikataba na bajeti ya taifa na mawazo yao kutumika katika kufanya marekebisho.
Alisema kipindi hiki ambacho bajeti ya 2017/18 inaanza kujadiliwa leo bungeni, ilitakiwa midahalo mbalimbali ifanyike vyuoni kuichambua, lakini kwa sasa ukifanya hivyo unaonekana umetumwa na vyama vya upinzani, kitu ambacho siyo sahihi.
Alisema miaka ya nyuma viongozi wa serikali walikuwa wanahudhuria katika Ukumbi wa Nkrumah katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kusikiliza mawazo ya wasomi, lakini kwa sasa vyuo vikuu vinatumika kama sehemu ya vijana kupata taaluma pekee.
Alisema Chadema imeamua kujitoa ili kupambana na taabu wanazopata wananchi kwa kuondoa ushabiki wa kisiasa.
“Chadema tumeamua kuhakikisha tunawaeleza wananchi ukweli hata kama siasa zimezuiliwa, lakini tutafanya siasa mpya za kutumia akili kubwa,” alisema Sumaye

No comments:
Write comments